KATIKA utekelezaji wa mikakati yake na hususani kwenye uwekezaji, Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) limeendelea kuhakikisha wajasiriamali wazalishaji wanapatiwa maeneo mazuri ya uzalishaji wa bidhaa zao.
Lengo ni kuhakikisha bidhaa za wajasiriamali zinazozalishwa zipo kwenye ubora unaotakiwa kitaifa na kimataifa.
Takribani majengo 20 yamejengwa katika mikoa mbalimbali kutokana na uhitaji mkubwa wa wajasiriamali wazalishaji. Hivi karibuni SIDO Tanga ilifanya ufunguzi rasmi wa jengo lake lililopo mtaa wa viwanda ambapo uzalishaji wa bidhaa mbalimbali utakuwa unafanyika.
Mikoa ambayo majengo haya yamejengwa ni pamoja na Kigoma, Geita, Chato, Simiyu, Katavi n Kagera. Majengo haya yana miundo mbinu mbalimbali zikiwemo umeme, maji na barabara, hii ni kwa ajili ya kuwarahisia kupokea malighafi, kuchakata, kusindika na hatimaye kusambaza bidhaa zao.
Baadhi ya wajasiriamali katika mikoa husika watafaidika na utumiaji wa majengo haya ikiwemo upatikanaji wa eneo la uzalishaji likiwa na miundombinu yote muhimu kwa bei nafuu.