NA DEVOTHA FULUGUNGE
MKAZI wa Salasala Hassan Bangaseka amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya Kinondoni, kwa tuhuma za kumlawiti mtoto wa kiume kinyume na maumbile.
Bangaseka (24), alifikishwa Mahakamani hapo jana mbele ya Hakimu Mkazi Upendo Ngitiri.
Awali, mwendesha mashitaka wa umma Hamis Said mbele ya Hakimu Ngitiri kupitia hati ya mashitaka alidai, tukio lilitokea Novemba 18, mwaka 2020 eneo la Kilongima wilayani Kinondoni jijini Dares Salaam.
Aliendelea kudai kuwa, mshitakiwa alifanya mapenzi kinyume cha maumbile na kijana wa kiume mwenye umri wa miaka 16 aliyejulikana kwa jina la Francis Leonard.
Mbali na hapo, Bangaseka alikana kutenda kosa mbele ya Mahakama na upande wa Jamhuri ulidai upelelezi umekamilika na kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya hoja za awali
Hakimu Ngitiri alisema dhamana iko wazi na kutaja masharti ya dhamana yaliyomtaka mshitakiwa kuwa na wadhamini wawili wenye barua za utambulisho na vitambulisho.
Aliendelea kusema kuwa, kila mdhamini angetakiwa kusaini bondi ya Shilingi laki nane.
Kwa kuwa mshitakiwa huyo alitimiza masharti ya dhamana Mahakama ilimuachia kwa dhamana hadi Januari 28, 2021 kwa ajili ya kusomewa hoja za awali.